Breaking

MADA YA TATU: MAPAMBANO YA AWALI DHIDI YA UVAMIZI WA KIKOLONI

  DHANA YA UVAMIZI WA KIKOLONI

Uvamizi wa kikoloni ni kitendo cha nchi moja kuingia katika nchi nyingine kwa lengo la kuanzisha utawala wake kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Ø  Mara nyingi uvamizi huu hutekelezwa kwa kutumia nguvu za kijeshi.

Ø  Uvamizi wa kikoloni nchini Tanzania (Tanganyika na Zanzibar) ulipingwa vikali kwa sababu jamii za kitanzania zilifahamu kwamba kuruhusu wakoloni kuvamia kungesababisha kupoteza uhuru wao.

Ø  Kwa sababu hiyo, viongozi wa jamii za kitanzania waliongoza mapambano dhidi ya uvamizi huo tangu miaka ya 1880 na mapambano hayo yaliendelea hata baada ya ukoloni kuanzishwa nchini Tanganyika.

Ø  Mapambano ya awali dhidi ya wakoloni yalihusisha jamii moja moja, yaani hayakuhusisha nguvu za pamoja za jamii mbalimbali za kitanzania kama taifa moja la Tanzania.

Ø  Mapambano hayo yalilenga kuzuia kuingizwa kwa maadili ya kikoloni katika jamii za kitanzania.

Ø  Wakoloni walileta maadili ya kibepari ikiwa ni pamoja na ubaguzi wa rangi, uporaji, ukatili, unyonyaji, unyanyasaji, matabaka, na ubinafsi.

Ø  Pia walileta maadili ya dini za kigeni (Ukiristo na Uislamu) ambayo mara nyingi yalipingana na maadili ya dini za jadi

 

SABABU ZA KUPINGA UVAMIZI WA KIKOLONI NA MAADILI YAKE

a)      Kupotea kwa uhuru, kudunishwa na kuharibiwa kwa maadili ya jamii.

Ø  Mila na desturi ambazo zilikuwa msingi wa maadili ya kiafrika zilidhihakiwa na wakoloni, hali hii ilichochea waafrika kuupinga uvamizi wa wakoloni ili kulinda uhuru, utamaduni na maadili yao.

b)     Unyonyaji na ukandamizaji wa kikoloni dhidi ya wananchi.

Ø  Wananchi walinyonywa kwa kulazimishwa kufanya kazi za vibarua na kulipwa ujira mdogo katika mashamba ya mkonge, pamba, chai, tumbaku na pareto.

Ø  Wakulima hao walidhalilishwa kwa kuchapwa viboko wakiwa mashambani.

c)      Kuanzishwa kwa mifumo mipya ya kodi kandamizi.

Ø  Wakoloni walianzisha mfumo wa ulipaji kodi kwa lazima, ikiwemo kodi ya kichwa, na nyinginezo kwa pesa taslimu.

Ø  Hivyo wananchi iliwalazimu kuuza mifugo pamoja na kufanya vibarua katika mashamba yao ili wapate pesa kwa ajili ya kulipa kodi hizo.

d)     Kuwepo kwa adhabu za kikatili  dhidi  ya wananchi.

Ø  Wakoloni walianzisha adhabu za kikatili kama vile kuwanyonga viongozi wa jamii za kitanzania waliopinga utawala na maadili yao.

Ø  Wananchi pia waliteswa na kudharirishwa hadharani waliposhindwa kulipa kodi au walipotenda makosa mengine.

Ø  Hali hii ilishusha heshima na utu wao, jambo lililochochea harakati za kupinga uvamizi wa kikoloni.

e)      Kuporwa kwa ardhi yenye rutuba.

Ardhi ya wananchi iliporwa kwa ajili ya kulima mazao ya biashara ya wakoloni, hali iliyofanya wananchi washindwe kukidhi mahitaji yao ya chakula kutokana na kuwa na mashamba madogo yasiyo na rutuba ya kutosha.

f)       Kulazimishwa kulima mazao ya biashara kwa faida ya wakoloni.

Pia wananchi walilazimishwa kulima mazao ya biashara kama pamba, kahawa na chai kwa faida ya wakoloni na mabepari wa ulayamagharibi, ambapo mazao hayo yaliuzwa kwa bei ndogo.

 

UPINZANI DHIDI YA UVAMIZI WA KIKOLONI KATIKA JAMII ZA KITANZANIA

Karibu jamii zote za kitanzania ziliupinga uvamizi wa kikoloni kwa sababu hakuna jamii iliyopenda kupoteza uhuru na utamaduni wake kwa wageni.

Uvamizi huo ulipigwa kwa njia ya vita, zingine kwa kujisalimisha na nyingine kwa kuungana na wavamizi

 

1.       NJIA YA KUPAMBANA KWA VITA

Ø  Njia ya vita ilikuwa maarufu zaidi kati ya jamii za kitanzania, kwani jamii nyingi hazikuwa tayari kupoteza uhuru wao na hivyo ziliupinga waziwazi uvamizi huo kwa kutumia vita.

Ø  Mapambano dhidi ya uvamizi wa kikoloni na maadili yake yalihusisha jamii moja moja au jamii nyingi kwa pamoja.

(a) Mapambano ya wanyamwezi

Ø  Harakati za kupinga uvamizi wa wajerumani magharibi mwa afrika mashariki ziliongozwa na mtemi wa Wanyamwezi aliyejulikana kama Isike au Mwana Kiyungi kuanzia mwaka 1886 hadi 1891.

Ø  Mtemi Isike alipinga vikali uvamizi wa wajerumani katika himaya yake baada ya maeneo yake ya kiutawala kuporwa. Pia alitetea masilahi ya kibiashara miongoni mwa jamii ya kinyamwezi huko Tabora.

Ø  Mtemi Isike aliwaongoza kwa ushupavu askari wake kupambana na wajerumani wenye wanajeshi zaidi ya 1000.

Ø  Hata hivyo ngome ya Isike ilivunjwa na wanajeshi wa kijerumani, na mtemi huyo alipoona ameelemewa aliona ajiue kuliko kukamatwa na wajerumani, hivyo alijilipua na baruti pamoja na familia yake mnamo mwaka 1893.

 

(b) Mapambano ya jamii za watu wa Pwani

Ø  Katika ukanda wa pwani ya Afrika Mashariki mapambano ya awali dhidi ya uvamizi wa kijerumani yaliongozwa na wafanyabiashara mashuhuri ambao ni:-

i.        Abushiri bin Salim al-Harthi wa Pangani

ii.      Bwana Heri bin Juma wa Uzigua.

Ø  Viongozi hawa waliongoza mapambano dhidi ya sera za unyonyaji za kijerumani.

Ø  Mwaka 1889, Abushiri bin Salim aliwaongoza wananchi wa pwani katika maeneo ya pangani kupigana na wajerumani na kufanikiwa kuwaondoa katika baadhi ya maeneo ya pwani.

Ø  Wajerumani hao waliomba msaada kwa majeshi ya uingereza, hali iliyosababisha Abushiri kukimbia kwa sababu za kiusalama.

Ø  Wajerumani walifanikiwa kumkamata Abushiri baada ya kusalitiwa na chifu Magaya wa Usagara. Mwaka 1889, Abushiri aliuawa kikatili kwa kunyongwa hadharani na wajerumani huko bagamoyo

 

Bwana Heri aliwaongoza wazigua maeneo ya Saadani dhidi ya uvamizi wa wajerumani.

Ø  Ingawa baadae alishindwa, alionesha mapambano makali ambayo yalionesha jinsi wananchi walivyokuwa hawako tayari kunyanyaswa na kunyonywa na wajerumani.

Ø  Kilwa Kivinje, mapambano dhidi ya wajerumani yaliongozwa na Hassan bin Omari Makunyanga mwaka 1894.

Ø  Hata hivyo makunyanga alikamatwa na kunyongwa na wajerumani huko kivinje kwenye mwembe ambao mpaka sasa unajulikana kama ‘mwembe wa kunyonga’

 

 

 

(c) Mapambano ya wahehe

Ø  Jamii ya wahehe chini ya uongozi wa Mtwa Mkwawa ilipinga vikali uvamizi wa wajerumani kati ya mwaka 1891 na 1898 kwa njia ya vita.

Ø  Wahehe walijiimarisha sana kwa kupanua maeneo yao na kutoza ushuru kwa wafanyabiashara waliopita kwenye maeneo yao.

Ø  Wajerumani walikasirishwa na kitendo cha wahehe kuendelea kujiimarisha kwa kuongeza maeneo kama usagara, mpwampwa na ugogo.

Ø  Wahehe walikuwa wanaendeleza nguvu zao kutoka Kalenga, ambayo ilikuwa ngome ya Mtwa Mkwawa hadi maeneo mengine.

 

Ø  Mapambano ya kwanza ya kijeshi kati ya wahehe na wajerumani yalifanyika mwaka 1891 katika eneo la Lugalo. Wanajeshi wa kijerumani chini ya kamanda Emil Von Zelewisky walitumwa kuangamiza wahehe.

Ø  Katika mapigano hayo, wanajeshi wa kijerumani walishindwa, takribani askari 300  wa kijerumani pamoja na kiongozi wao waliuawa.  

Ø  Mwaka 1894, wajerumani chini ya kamanda Tom Prince walivamia ngome ya wahehe huko Kalenga. Mkwawa alikimbilia mafichoni na kuendelea na vita vya msituni.

Ø  Mwaka 1898, Mtwa Mkwawa aliamua kujiua kwani aliona ni fedheha kwa shujaa kukamatwa na kunyongwa hadharani na wavamizi.

 

(d) Mapambano ya wayao

Ø  Kwa upande wa kabila la wayao mapambano yaliongozwa na kiongozi wao jasiri na shupavu aliyeitwa Mwene Machemba.

Ø  Kiongozi huyu alishinda karibu mapambano yote aliyoyaongoza dhidi ya wajerumani.

Ø  Mwene machemba alikuwa kiongozi hodari, shupavu na mwenye kupenda kutetea maadili na uhuru wa watu wake.

Ø  Kwa mfano katika barua aliyowaandikia wajerumani, Mwene Machemba alisema ’nimesikiliza maneno yenu, lakini sijaona sababu ya kuwatii. Niko tayari kufa…, sisemi mnitii mimi kwa kuwa nyie ni watu huru kama mimi’’

Ø  Hata hivyo Machemba alikimbilia msumbiji baada ya kupambana vikali na majeshi ya kijerumani, ambapo wayao walizidiwa nguvu na kushindwa vita.

 

(e) Mapambano ya wachaga

Ø  Katika jamii ya wachaga, mapambano dhidi ya uvamizi wa kikoloni yaliongozwa na:-

i.        Mangi Sina wa Kibosho

ii.      Mangi meli wa Moshi.

Ø  Huko kibosho walipinga kitendo cha wajerumani kuingilia mgogoro uliokuwepo miongoni mwa watawala wa Kibosho, Moshi na Marangu.

Ø  Kitendo hicho kilimuudhi Mangi Sina na kuamua kuichana bendera ya Wajerumani jambo lililowakasirisha wajerumani, ambao walitumia majeshi ya kukodi ya wanubi kutoka Sudani ili kupambana naye.

Ø  Hata hivyo, baada ya kuzidiwa nguvu na wajerumani, Mangi Sina alilazimika kutoroka.

 

Ø  Mangi Meli aliongoza mapambano huko Moshi dhidi ya majeshi ya kijerumani.

Ø  Katika mapambano hayo, Kamanda wa jeshi la wajerumani, Von Bulow, aliuawa.

Ø  Kwa kulipiza kisasi, wajerumani walimshambulia Mangi Meli, wakamkamata na baadaye wakamnyonga kwa ukatili kijijini kwake.

 

(f) Vita vya Liti Kidanka dhidi ya wajerumani (1908-1910)

Ø  Wajerumani walifika singida mnamo mwaka 1901.

Ø  Wajerumani walikabiliana na upinzani mkali kutoka kwa wanyanturu, walioongozwa na mwanamke shupavu, Liti Kidanka, kupinga uvamizi huo.

Ø  Liti kidanka hakutaka wajerumani watawale eneo ambalo sasa ni mji wa singida.

Ø  Hivyo aliongoza mapambano makali dhidi ya askari wa kijermani walioongozwa na Kapteni Eberhard von Sick

Ø  Liti na askari wake walipambana na wajerumani mara mbili na kufanikiwa kuwakimbiza nje ya mji wa singida kwa kutumia mbinu ya kipekee ya silaha ya nyuki wakali.

Ø  Nyuki walifunguliwa kipindi cha mapigano na kuwashambulia askari wa kijerumani pekee.

Ø  Mapigano hayo yalidumu kwa miaka mitatu, kuanzia mwaka 1908 hadi 1910

Ø  Hata hivyo, katika jaribio la tatu na la mwisho, Liti Kidanka hakufanikiwa kuwashinda wajerumani kutokana na kusalitiwa na mmoja wa washirika wake. Hivyo alikamatwa yeye na mume wake na kuuawa. Kichwa cha shujaa huyu kilikatwa na kupelekwa ujerumani.

 

(g) Mapambano ya jamii za kusini mwa Afrika mashariki ya kijerumani (Vita vya maji maji)

Ø  Mapambano ya jamii za kusini, yajulikanayo kama vita vya maji maji yalianza mwaka 1905 na kumalizika mwaka 1907.

Ø  Kiongozi wao alikuwa ni Kinjekitile Ngwale wa kabila la wamatumbi, ambaye aliwaongoza wamatumbi kupinga ukatili, unyonyaji na ukandamizaji wa wajerumani.

Ø  Kinjekitile alidai kuwa ameoteshwa dawa ambayo ingewaepusha na risasi za wajerumani.

Ø  Dawa hiyo ilikuwa ni mchanganyiko wa maji na mtama, yaliyodaiwa kuwa na uwezo wa kuzigeuza risasi kuwa maji.

Ø  Wanajamii waliamini ahadi zake na vita ilipoanza, wakoloni waliporusha risasi, wao walitamka maji, hata hivyo, kadri walivyosema maji ndivyo walivyopoteza maisha.

Ø  Vita hivi vilienea katika maeneo ya kusini na mashariki mwa afrika kama vile Rufiji, Mohoro, Somanga, Kibata, Nandete, Mikindani, Liwale, Lindi, Songea, Njombe, na Mahenge.

Ø  Kinjengitile alitumia mbinu hii kuwaunganisha na kujenga mshikamano miongoni mwa wananchi ili wapambane na mkoloni bila hofu.

 

2.      KWA NJIA YA KUUNGANA

Ø  Kuna jamii za kitanzania zilijua nguvu ya kijeshi ya wajerumani na hawakuwa tayari kupambana na kuupinga uvamizi wao moja kwa moja. Lakini waliungana ili kuweza kuwashinda maadui wao.

 

Sababu za kuungana na Wakoloni.

i.        Imani kwamba, baada ya kuwashinda maadui wao wa muda mrefu wangebaki kuwa na nguvu zaidi na kujiimarisha.

ii.      Kupata misaada ya silaha na vifaa vingine kutoka kwa wajerumani.

iii.    Nguvu ndogo ya kijeshi kwa jamii za Kitanzania

Ø  Mfano wa jamii hizi za kitanzania ni kama vile wachaga ambao walikuwa chini ya Mangi Mandara waliungana ili kumshinda Mangi Sina, Wasangu na wabena waliungana na wajerumani kupambana na Mtwa Mkwawa wa wahehe

Ø  Ukweli ni kwamba jamii hizi zote zilishindwa kupata walichokitarajia na mwisho kutawaliwa kirahisi na wajerumani.

Ø  Hivyo, usaliti wao dhidi ya watawala wa jamii za kitanzania kwa kuungana na wajerumani ulikuwa ni fedheha kwao kwani hakukuwa na manufaa yoyote.

 

3.      KWA NJIA YA KUSALIMU AMRI

Ø  Kuna baadhi ya jamii za kitanzania ambazo hazikupenda kutawaliwa na wakoloni lakini zilijiona hazina uwezo wa kupambana nao kivita.

Sababu za kusalimu amri mbele ya Wakoloni.

i.        Atahari zilizotokana na baa a njaa au magonjwa

ii.      Ukosefu wa dola zenye nguvu

iii.    Mazingira magumu ya kivita n.k

Ø  Mfano jamii za kimasai hapa nchini ilisalimu amri kwa wajerumani kufuatiwa kupatwa na majanga ya magonjwa ya wanyama miaka ya 1870s na 1880s na mazingira yake kutokuwa mazuri kwa vita

 

CHANGAMOTO ZILIZOKABILI MAPAMBANO DHIDI YA UVAMIZI WA KIKOLONI

Ø  Wananchi walijaribu kupambana na kupinga ukoloni, lakini wakoloni waliwazidi nguvu na kuwashinda.

Zipo sababu nyingi zilizowafanya wananchi kushindwa katika mapambano hayo, miongoni mwa sababu hizo ni kama zifuatazo;

a)      Ukosefu wa umoja miongoni mwa jamii za kitanzania.

Katika kipindi cha ukoloni, jamii za kitanzania zilishindwa kwa sababu zilikosa umoja na hazikushirikiana kupambana na wakoloni.

Ø  Kwa mfano katika vita vya maji maji, makabila hayakuungana yote kwa pamoja kila kabila lilipigana kivyake katika eneo lake

b)     Matumizi ya silaha duni dhidi ya silaha bora za wajerumani.

Silaha zilizotumiwa na jamii za kitanzania zilikuwa duni sana. Wajerumani walitumia mizinga na bunduki, wakati wananchi walitumia pinde, mishale, ngao, mawe, marungu na majambia

c)      Usaliti.

Baadhi ya viongozi wa jadi waligeuka kuwa vibaraka wa serikali ya kikoloni.

Ø  Mfano wasangu na wabena waliungana na wajerumani kutoa siri na kupigana na wahehe. Vivyo hivyo katika jamii za kichaga Mangi Mandara/ Rindi waliungana na wajerumani kumshinda Mangi Sina

d)     Maandalizi duni;

Wananchi hawakuwa na maandalizi mazuri ya vita ikilinganishwa na wajerumani.

Ø  Wavamizi walikuwa na muda mzuri wa kujiandaa kwa vita, wakati jamii nyingi za Kitanzania zilijikuta katika vita ghafla baada ya kuona wavamizi tayari wameshaingia.

Ø  Pia jamii za Kitanzania zilikuwa hazijamjua vizuri adui yao jambo lililochangia kushindwa kwao.

 

 

e)      Teknolojia duni ya mawasiliano;

Watanzania walitumia njia za jadi katika mawasiliano na zilitumia muda mrefu kufikisha taarifa kwa walengwa. Hii ilipelekea ugumu wa mawasiliano wakati wa vita.

Ø  Wajerumani walikuwa na teknolojia nzuri ya mawasiliano na usafiri, ambayo ilirahisisha mawasiliano kati ya maeneo mbalimbali, mfano matumizi ya telegram kutuma taarifa za vita kuhusu vifaa na wanajeshi kwa haraka. Pia wajerumani walitumia magari huku watanzania wakitembea kwa miguu.

f)       Uchumi dhaifu;

Ø  Jamii nyingi za kitanzania zilikuwa na uchumi dhaifu ambao usingeweza kuhimili vita kwa muda mrefu.

Ø  Wakati huohuo Wajerumani walikuwa na uchumi imara uliowawezesha kuhimili vita kwa muda mrefu kwani nchi ya ujerumani ilikuwa na uwezo wa kuwasidia kifedha.

 

MATOKEO YA KUPINGA UVAMIZI WA KIKOLONI

Ø  Ni muhimu kukumbuka kuwa jamii za kitanzania zilipambana vikali kuupinga ukoloni. Kutokana na matumizi ya silaha duni za jadi, wakoloni walifanikiwa kuzishinda na kuzitawala. Katika kipindi chote cha vita, wananchi walijitoa kwa hali na mali wakiongozwa na viongozi wao wa jadi waliotetea uhuru, haki, masilahi na utu wao.

Matokeo ya mapambano hayo ni kama ifuatavyo

i.        Kusimama kwa shughuli za uzalishaji mali;

Kipindi chote cha vita badala yz kuzalisha muda mwingi ulitumika kujipanga kivita na kupigana.

Ø  Hali hii ilisababisha upungufu wa chakula na kuleta njaa kubwa, njaa hii iliitwa ‘Fungafunga’ huko kusini kwenye vita vya maji maji.

Ø  Watu wengi walikula wadudu, mizizi na matunda ya msituni ambayo baadhi yalikuwa na sumu

ii.      Kutumikishwa kwa nguvu kazi ya vijana;

Wanaume hasa vijana wenye nguvu walisafirishwa mbali na makazi yao na kutumikishwa katika mashamba ya walowezi.

iii.    Watu kuyaacha au kuyakimbia makazi yao

Wakati wa vita, wapiganaji walitumia muda mwingi msituni. Wanawake na watotot pia walikimbilia msituni na kwenye mapango ili kujificha.

Ø  Hali hii ilipelekea wengine kujeruhiwa na wengine kuuawa na wanyama wakali wa msituni

 

iv.    Hofu miongoni mwa watanzania;

Vita vilisababisha kujengeka kwa hofu miongoni mwa watanzania. kutokana na kushindwa kwa mapambano, watu wengi walipata hofu ya kupigana tena na wazungu jambo ambalo lingepoteza uhai wao.

v.      Mateso na vifo vingi vya watu.

Vita vya kupinga uvamizi wa wakoloni vilisababisha maelfu ya vifo vya watu katika mapambano, kukamatwa kwa mateka, kunyongwa nakadhalika.

Ø  Pia baadhi ya vifo vilitokana na njaa wakati na baada ya vita.

vi.    Mwamko mpya wa harakati za uhuru;

Baada ya kushindwa kwenye vita hivo, jamii nyingi za kitanzania zilionesha ujasiri na dhamira ya kweli ya kupinga ukandamizaji wa kigeni.

Ø  Hali hii ilichochea mwamko mpya wa wapigania uhuru wa baadae, ambao walijifunza mengi kutoka kwa harakati hizo za kitaifa za kudai uhuru

vii.  Kumbukumbu muhimu katika historia ya Tanzania;

Vita vya kupinga ukoloni ni kumbukumbu muhimu katika historia ya Tanzania inayostahili kuheshimiwa na yeyote anayethamini utu, uhuru, haki, heshima na usawa.

Ø  Vita hivyo ni kielelezo halisi cha Watanzania katika kukataa utawala wa kikoloni.

Ø  Vita hivyo vinatukumbusha kuwa tunapaswa kuwa na ushujaa na uzalendo kama ilivyokuwa enzi za mababu na mabibi zetu.

 

ZOEZI

1)      Tofautisha kati ya maadili ya kikoloni na maadili ya jamii za kitanzania

2)      Eleza sababu tano (5) za kushindwa kwa mapambano ya awali ya jamii za kitanzania dhidi ya uvamizi wa kikoloni

3)      Eleza jinsi viongozi wa sasa wanapaswa kutetea masilahi ya wanachi kwa ujasiri na uzalendo



No comments:

Post a Comment