Breaking

MADA YA SITA: MAPINDUZI MATUKUFU YA ZANZIBAR

 DHANA YA MAPINDUZI:

Mapinduzi katika mktadha huu yanarejerea harakati za kubadili utawala wa kisiasa, ndani ya muda mfupi kwa kutumia nguvu za kijeshi au nguvu za umma.

Ø  Mapinduzi yanahusisha kuiondoa serikali au mfumo wa utawala uliopo  na kuweka mwingine.

AINA ZA MAPINDUZI

Kuna aina kuu mbili za mapinduzi ambazo ni kama ifuatavyo

i. Mapinduzi ya kisiasa

ii. Mapinduzi ya kijeshi

 

i.                    Mapinduzi ya kisiasa

Ø  Ni mapinduzi yanayofanywa kupitia nguvu za umma.

Ø  Katika mapinduzi haya, wananchi walio wengi na wanyonge huwaondoa watawala wachache kwa kuzitumia nguvu za umma, mara nyingi bila kumwaga damu kwa kiasi kikubwa.

Ø  Wananchi wanaweza kutumia njia za maandamano n.k

ii.                  Mapinduzi ya kijeshi

Ni mapinduzi ambayo hufanywa na jeshi kwa lengo la kuondoa utawala uliopo madarakani kwa kutumia mapigano au mbinu za kijeshi

Mfano wa mapinduzi ya kijeshi ni kama ifuatavyo

·         Mapinduzi ya kijeshi Misri yakiongozwa na Kanali Gamal Abdel Nasser dhidi ya Mfalme Farouk I mwaka 1952

·         Mapinduzi ya kijeshi Ethiopia yakiongozwa na Mengistu Haile Mariam dhidi ya Haile Selassie mwaka 1974

·         Mapinduzi ya Jenerali Iddi Amin Dada wa Uganda dhidi ya Rais Milton Obote mwaka 1971

 

CHIMBUKO LA MAPINDUZI MATUKUFU YA ZANZIBAR

Ø  Zanzibar ilikuwa chini ya utawala wa kisultani hadi mwaka 1890.

Ø  Sultan Seyyid Saidi alikuwa sultani wa kwanza kuongoza dola mbili, yaani Omani na Zanzibar akiifanya Zanzibar kuwa makao makuu ya himaya hizo.

Ø  Sultani huyo alihamia Zanzibar akitokea Muscat, Oman mnamo mwaka 1840.

Ø  Mnamo mwaka 1890, Zanzibar iliwekwa chini ya watawala wa Waingereza na ikatambulika kama mahamia ya Uingereza au ‘’British Protectorate’’.

Ø  Katika hali hiyo, waingereza walitumia utawala wa sultani katika kuitawala Zanzibar.

 

Waingereza walitoa uhuru kwa Zanzibar tarehe 10 Desemmba 1963.

Uhuru huu ulikuwa wa serikali ya mseto wa vyama vya ZNP na ZPPP. Uhuru huu haukuungwa mkono na waafrika wengi maana waliona kuwa uhuru umetolewa kwa waarabu badala ya wananchi wote

Ø  Mapinduzi matukufu ya Zanzibar yalikuwa ni kilele cha harakati za mapambano ya ukombozi wa wazanzibar.

Ø  Mapambano haya yalikuwa ni matokeo ya uchaguzi na uhuru uliotolewa tarehe 10 Desemba 1963 chini ya serikali ya waziri mkuu Mohammed Shamte na Sultan Jamshid bin Abdullah Al Said, uhuru ambao ulijulikana kama ‘’uhuru wa wachache’’,

Ø  Hivyo, kufikia tarehe 12 January 1964, yalifanyika mapinduzi rasmi Zanzibar chini ya uongozi wa mwanamapinduzi Sheikh Abeid Amani Karume, ambaye aliongoza Zanzibar kuanzia mwaka 1964 hadi alipouawa tarehe 7 April 1972.

 

SABABU ZA MAPINDUZI MATUKUFU YA ZANZIBAR

Ø  12 Januari 1964, mapinduzi matukufu ya Zanzibar yalifanyika. Sababu zilizosababisha mapinduzi Zanzibar ni kama ifuatavyo;

 

A: SABABU ZA KISIASA

i.                    Kuondolewa kwa utawala wa wenyeji

Kabla ya utawala wa waarabu, wazanzibari walikuwa na viongozi wao kama vile mwinyi mkuu kwa upande wa Unguja na Makamandume kwa upande wa Pemba.

Ø  Baada ya kuja kwa utawala wa wageni hasa kipindi cha usultani wa Waarabu watawala wa kienyeji waliondolewa katika utawala.

Ø  Kuanzia wakati wa usultani wa Waarabu hadi ukoloni wa waingereza, masilahi ya wenyeji hayakuzingatiwa wala hayakupewa kipaumbele.

Ø  Mfano; Wenyeji hawakushirikishwa kwenye vyombo vya kutoa maamuzi au kuwa viongozi serikalini.

ii.                  Ubaguzi katika Baraza la kutunga sharia.

Vilevile kwenye baraza la kutunga sharia, Waafrika wachache walipata nafasi ukilinganisha na Waarabu na Wahindi.

Ø  Hivyo wajumbe hawa wachache hawakuweza kutetea masilahi ya waafrika walio wengi Zanzibar.

Ø  Kwaiyo Wazanzibar hawakupata uhuru wa kujitawala na kufanya maamuzi yao wenyewe.

iii.                Udanganyifu na vurugu za uchaguzi.

Chaguzi zote tatu zilizofanyika Zanzibar zilitawaliwa na mizengwe iliyosababisha kukataliwa kwa matokeo.

Ø  Mfano, Uchaguzi wa Julai, 1963 ambao ulimfanya Mohamed Shamte kuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Zanzibar ulionekana ni upendeleo na kuendeleza ubaguzi.

 

B: SABABU ZA KIJAMII

i.                    Mfumo wa kibaguzi wa kikoloni katika masuala ya kijamii.

Huduma za kijamii kama vile elimu, maji, umeme na afya zilitolewa kwa ubaguzi.

Ø  Kwa mfano, Mwaka 1955, asilimia 14 ya bajeti ya serikali katika elimu ilielekezwa kwenye shule za Wahindi wakati kipindi hicho Wahindi walikuwa asilimia 6 tu ya wakazi wa Zanzibar.

Ø  Huduma za maji safi na umeme ziliimarishwa katika maeneo ambako Waarabu, Wahindi na Wazungu waliishi.

Ø  Hivyo ubaguzi katika Nyanja mbalimbali ulileta chuki na kusababisha kuzuka kwa Mapinduzi ya Zanzibar mnamo January, 1964.

 

ii.                  Kutozingatiwa kwa maadili ya wenyeji.

 Maadili ya kuheshimu watu wa rika na tabaka zote hayakuzingatiwa.

Ø  Watu walianza kuheshimiwa kutokana na vyeo na asili yao (rangi)

 

C: SABABU ZA KIUCHUMI

i.        Unyang’anyi wa rasilimali za wenyeji kama vile ardhi.

Ø  Wazanzibar wengi walinyang’anywa ardhi yao yenye rutuba na kubaki vibarua katika mashamba ya wageni.

ii.                  Kutawala kwa Wahindi katika biashara.

Ø  Wahindi walitawala biashara zote za jumla na rejareja madukani wakiwa pamoja na Waarabu.

iii.                Kuathirika kwa shughuli kama vile kilimo, uvuvi na ufugaji.

Ø  Ujio wa wakoloni uliathiri shughuli nyingi za uchumi za wazanzibar kama vile kilimo, uvuvi, ufugaji n.k. wakoloni walichukua rasilimali kama ardhi zenye rutuba, minazi na mikarafuu kwa manufaa yao binafsi na ya ukoloni

 

MCHANGO WA MAPINDUZI MATUKUFU YA ZANZIBAR

Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964 yalileta mabadiliko makubwa katika historia ya Zanzibar na yalikuwa na athari kubwa katika ukanda wa Afrika mashariki na maeneo mengine. Mapinduzi hayo yalisababisha kuondolewa kwa utawala wa kisultani na kuanzishwa kwa serikali iliyoongozwa na wazalendo wa chama cha Afro-Shirazi Party (ASP), Chama kilichoongozwa kwa misingi ya utu, haki na ustawi wa watu wote bila kuzingatia tofauti za asili, hadhi u kabila.

Michango ya mapinduzi ya Zanzibar ni kama ifuatavyo;

 

a) Kujenga umoja

Mapinduzi yalisaidia kuvunja migawanyiko na chuki zilizojengwa kutokana na hali ya ubaguzi katika jamii wakati wa ukoloni.

Ø  Hii ilidhihirishwa pale ambapo rais wa Jamhuri ya watu wa Zanzibar alipotangaza wajumbe 29 wa baraza la kwanza la mapinduzi Zanzibar.

Ø  Baraza hili lilikuwa na jukumu la kuunda upya taifa lenye umoja, haki na kuondoa ubaguzi uliokuwa umeota mizizi kwa miaka mingi visiwani Zanzibar.

Ø  Lakini pia mapinduzi ya Zanzibar yalichochea muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika na hatimaye kuundwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 1964

b) Kujenga mshikamano

Mapinduzi ya Zanzibar yalichangia kwa kiasi kikubwa kuleta mshikamano baina ya wananchi.

Ø  Hii ni kwa sababu ya kuundwa kwa serikali inayowakilisha makundi yote ya kijamii pamoja na kuondoa mgawanyiko wa kikabila na kidini

Ø  Aidha serikali ya mapinduzi Zanzibar ilipitisha kanuni za ujamaa na udugu ambazo zilisisitiza usawa, umiliki wa pamoja wa rasilimali na mshikamano.

Ø  Huduma za jamii kama vile elimu, afya na makazi zilitolewa kwa usawa bila kujali rangi, kabila au dini.

Ø  Vilevile mapinduzi ya Zanzibar yalichochea hisia ya fahari ya kitaifa, uzalendo na kujitolea kwa manufaa ya wote, ambayo yameendelea kujenga mfumo wa maadili wa taifa hadi sasa

c) Ujenzi wa maadili

Mapinduzi ya Zanzibar yalileta ukomo wa matabaka yote yaliyokuwepo kati ya waarabu, wahindi na waafrika.

Ø  Serikali mpya ilisisitiza umuhimu wa demokrasia, haki za binadamu, utu, usawa na ustawi wa watu.

Ø  Hii ilichangia katika kuhifadhi maadili ya jamii kama vile ushirikiano, usawa, kuheshimiana na kusaidiana ambayo ni sehemu muhimu ya utamaduni na utambulisho wa Mzanzibari.

Ø  Sambamba na hayo, mapinduzi pia yalisaidia kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili. Kiswahili kilikuwa lugha rasmi ya serikali na wananchi wote wa Zanzibar.

 

ZOEZI

1.      Bainisha jitihada zingine zilizochukuliwa na serikali ya mapinduzi ya Zanzibar katika kuujenga umoja, usawa na mshikamano kwa jamii za wazanzibari.

2.      Eleza ni kwa namna gani lugha ya Kiswahili imefanikiwa kuwaunganisha wazanzibari baada ya mapinduzi

3.      Fafanua namna mapinduzi matukufu ya Zanzibar yanavyoenziwa katika jamii ya sasa ya watanzania.

 

MADA YA KWANZA:UKOLONI KATIKA JAMII ZA KITANZANIA

MADA YA PILI:UKOLONI KATIKA JAMII ZA KITANZANIA

MADA YA TATU: MAPAMBANO YA AWALI DHIDI YA UVAMIZI WA KIKOLONI

MADA YA NNE: HARAKATI ZA KUDAI UHURU WA TANGANYIKA NA ZANZIBAR

MADA YA TANO: UJENZI WA TAIFA BAADA YA UKOLONI

MADA YA SITA: MAPINDUZI MATUKUFU YA ZANZIBAR


No comments:

Post a Comment