Breaking

MADA YA TANO: UJENZI WA TAIFA BAADA YA UKOLONI

DHANA YA UJENZI WA TAIFA:

Ujenzi wa taifa ni mchakato unaohusisha juhudi za pamoja za kuunda taifa jipya lenye utambulisho wake kupitia mifumo ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni, unaozingatia haki, usawa na demokrasia.

Ø  Katika taifa la Tanzania, mfumo huu ulijengwa juu ya misingi ya kifkra, kiitikadi, falsafa na maadili ya jamii za Kitanzania.

Ø  Harakati za ujenzi wa taifa zilikuwa muhimu kwa sababu ukoloni uliacha jamii iliyogawanyika, yenye ukosefu wa miundombinu muhimu, rasilimali watu na pia tofauti za kiuchumi na kijamii miongoni mwa wananchi.

 

MIFUMO ILIYIJENGWA KATI YA MWAKA 1961 HADI 1966

Ø  Uhuru wa Tanganyika wa desemba 9, 1961, pamoja na Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya januari 12, 1964, yaliashiria mwanzo wa ujenzi wa mifumo mipya ya kisiasa, kijamii, kiutamaduni na kiuchumi kwa taifa huru la Tanzania.

Ø  Mifumo hiyo ilijengwa chini ya Mwl JK Nyerere wa TANU pamoja na Abeid Amani Karume wa ASP.

Ø  Aidha , umoja ,uzalendo, kujitolea na kupenda kazi vilikuwa miongoni mwa maadili yaliyojengwa, yakiongozwa na kauli mbiu iliyotangaza vitu dhidi ya maadui watatu:

·         umaskini,

·         ujinga

·         maradhi.

Ø  Mifumo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii iliyojengwa katika kipindi hiki imefafanuliwa vema katika sehemu zinazofuata.

 

KISIASA

1.      Tanganyika kuwa Jamhuri

Ø  Tanganyika ilikuwa Jamhuri mwaka 1962.

Ø  Jamhuri ni serikali ya watu yenye mamlaka kamili, inayoongozwa na Rais.

Ø  Kabla ya Tanganyika kuwa jamhuri, serikali ilikuwa inaongozwa na Mwalimu JK Nyerere kama waziri mkuu , aliyekuwa chini ya mamlaka ya malkia wa uingereza, huku Gavana wa kikoloni akiendelea kuwa kiongozi mkuu wa nchi, akimwakilisha malkia Elizaabeth II wa Uingereza.

 

SABABU ZA TANGANYIKA KUWA JAMHURI

i.           Hitaji la kuwa na uhuru kamili wa serikali,

Ø  Hii ni kwa sababu kabla ya Tanganyika kuwa jamhuri, nchi ilikuwa na uhuru wa bendera chini ya uongozi wa malkia wa uingereza akiwakilishwa na Gavana.

Ø  Gavana huyo aliendelea kutekeleza baadhi ya majukumu ya kiserikali hivyo kumfanya waziri mkuu kukosa mamlaka kamili

ii.         Tanganyika ilitaka kutambulika katika jumuiya za kimataifa kama nchi yenye uhuru kamili.

Ø  Hivyo kuwa jamhuri ilikuwa njia ya kufanikisha hilo, kwani iliwapa fursa ya kushiriki katika mikutano ya jumuiya hizo za kimataifa kama nchi kamili.

iii.       Kupata uwezo wa kuingia mikataba ya kimataifa kama nchi huru yenye mamlaka yake kamili.

Ø  Wananchi walitakaSerikali ya jamhuri ili kuwa na uwezo wa kuingia mikataba ya kimataifa kama nchi huru yenye mamlaka yake kamili.

iv.       Kuwaondoa Wazungu katika nafasi za uongozi wa juu.

Ø  Lengo lilikuwa ni kuruhusu Watanganyika kushika madaraka ya uongozi katika taifa lao.

Ø  Kwani kabla ya kuwa jamhuri, Waingereza walikuwa bado wameshikilia nafasi za uongozi hali iliyowafanya Watanganyika wajihisi kuwa bado wapo chini ya utawala wa kikoloni.

v.         Kuwapa uhuru wananchi na viongozi kujitawala na kuharakisha maendeleo ya taifa.

Ø  Wananchi wa Tanganyika walitaka kufanya maamuzi bila kuingiliwa na wakoloni, kwani viongozi wa serikali hawakuwa na uhuru wa kufanya maamuzi ya kiutawala kabla ya jamhuri.

HIVYO;

v  Baada ya Tanganyika kuwa Jamhuri mwalimu Nyerere aliunda baraza la mawaziri.

 

2.      Kuanzishwa kwa sera ya Afrikanaizesheni

Ø  Hii ni sera iliyowapa madaraka watanganyika na wazanzibari wazawa.

Ø  Sera hii ililenga kutoa nafasi za uongozi na ajira kwa wazawa ambazo awali zilikuwa zikishikiliwa na wazungu na waasia wakati wa utawala wa kikoloni.

Ø  Watanganyika na wazanzibari wenye ujuzi walihamasishwa kufanya kazi serikalini na katika mashirika ya umma.

 

3.      Kuanzishwa kwa mifumo ya ulinzi na usalama

Ø  Ulinzi na usalama wa nchi pia ulitiliwa mkazo na serikali katika kujenga taifa.

Ø  Mfumo huu ulianzia ngazi ya chini kupitia mfumo wa ubalozi wa nyumba kumi.

Ø  Ili kuimarisha ulinzi na usalama, Jeshi la wananchi wa Tanzania (JWTZ) liliundwa mwaka 1964.

Ø  Tanzania ilirithi jeshi la kikoloni lililojulikana kama King’s African Rifles (KAR) ambapo nafasi nyingi za juu zilikuwa zikishikiliwa na wazungu na Waasia. Baada ya uhuru, jeshi hili lilibadilishwa jina na kuitwa Tanganyika Rifles (TR) Hadi mwaka 1964 lilipoanzishwa JWTZ.

Ø  Baada ya kuanzishwa kwa JWTZ, serikali ikawa makini kuteua na kuchagua watu waliounda jeshi jipya.

Ø  Kwa sehemu kubwa, jeshi hili liliundwa na vijana watiifu, waadilifu na wazalendo kutoka chama cha TANU na ASP. Bregedia Mirisho Sam Hagai Sarakikya aliteuliwa kuwa mkuu wa majeshi.

 

4.      Muungano wa Tanganyika na Zanzibar

Ø  Tarehe 26 Aprili, 1964, ni tukio muhimu la kihistoria na kisiasa katika kipindi hcho.

Ø  Muungano huu ulitokana na uhusiano wa kihistoria uliokuwepo kati ya jamii za Tanganyika na Zanzibar, uhusiano uliotokana na kiasi kikubwa cha udugu, historia na biashara uliojengwa karne nyingi kabla ya ukoloni.

Ø  Aidha, muungano huu ulikuwa nguzo muhimu katika kulinda uhuru na Mapinduzi matukufu ya Zanzibar. Muungano huu uliunda utaifa mpya wa Utanzania.

 

5.      Uanzishwaji wa mfumo wa chama kimoja cha kisiasa mwaka 1965

Ø  Tanzania iliamua kufuta mfumo wa vyama vingi na kuanzisha mfumo wa chama kimoja.

Ø  Vyama vilivyoruhusiwa kufanya siasa ni TANU kwa Tanganyika na ASP kwa Zanzibar.

Ø  Sababu ya kuanzishwa kwa mfumo wa chama kimoja ilikuwa ni kuleta maendeleo na kudumisha umoja na mshikamano. Uanzishwaji wa mfumo huu ulienda sambamba na uanzishwaji wa siasa ya ujamaa na kujitegemea mwaka 1967

 

UCHUMI NA HUDUMA ZA JAMII

Ø  Mara baada ya uhuru, serikali iliweka mkazo katika kujenga mifumo imara ya uchumi na huduma za jamii.

Ø  Harakati za kujenga mifumo hii ziliongozwa na nadharia ya kupambana na maadui watatu:

·         Ujinga,

·         Maradhi

·         Umasikini.

UCHUMI:

Ø  Mara baada ya uhuru, Tanganyika na Zanzibar zilirithi mfumo wa uchumi wa kikoloni ambao ulinufaisha watu wachache, hasa wageni.

Ø  Maendeleo yalikuwa ni hafifu katika sekta za biashara na viwanda.

Ø  Kulihitajika kujenga mfumo mpya wa uchumi. Mifumo ya uchumi iliyobuniwa katika kipindi hiki ililenga kujenga jamii ya watu wanaojitegemea.

 

        i.            Mpango wa maendeleo wa miaka mitatu uliotekelezwa kuanzia mwaka 1961 hadi 1964.

      ii.            Mpango wa kwanza wa maendeleo wa miaka mitano (1964-1969).

    iii.            Kuanzia mwaka 1963, sera ya maendeleo ya vijijini ilianzishwa.

Ø  Sera hii ililenga kuwaweka wananchi katika vijiji ili kuimarisha kilimo kwa kutumia teknolojia ya kisasa.

Ø  Wananchi walihimizwa kulima mazao ya chakula na biashara. Kupitia uhamasishaji huu, walipatiwa pembejeo na kupewa uhakika wa masoko ya mazao yao kupitia vyama vya ushirika

 

Ø  Vile vile viwanda mbalimbali vilijenga Tanganyika, mfano kiwanda cha nguo cha urafiki mwaka 1966

Ø  Aidha, serikali ilijikita katika kuhakikisha taasisi za fedha zinaendelezwa ili kuwa mihimili muhimu katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya taifa. Serikali ilianzisha benki kuu ya Tanzania mwaka 1966 ili kusimamia masuala muhimu ya kifedha nchini. Pia sekta nyingine,kama uvuvi, nishati na mdini zilipewa kipaumbele.

 

HUDUMA ZA JAMII

Ø  Mabadiliko katika utoaji wa huduma za jamii yalilenga kubadilisha mfumo wa kikoloni na kuunda mfumo unaokidhi mahitaji ya taifa huru.

Ø  Mfumo mpya wa utoaji huduma za jamii ulilenga kujenga jamii yenye ujuzi , maarifa na afya katika ujenzi wa taifa huru.

a.      Elimu.

Ø  Serikali iliandaa wataalamu wengi zaidi baada ya wazungu kuondoka

Ø  Shule nyingi zilijengwa na kuongeza idadi ya wanafunzi.

Ø  Elimu ilitolewa kwa watu wote bila kujali jinsia, dini au kabila.

Ø  Vyuo vya ufundi vilianzishwa, mfano chuo cha ufundi Dar es Salaam, ambacho kilipanuliwa mwaka 1962 na kuanza kutoa elimu ya ufundi mwaka 1964.

Ø  Vyuo vya ualimu pia vilianzishwa, mfano chuo cha walimu Morogoro.

 

b.      Afya

Ø  Zahanati na hospitali za umma vijijini na mijini vilijengwa. Mfano hospitali ya muhimbili ilipanuliwa zaidi mwaka 1961 mara tu baada ya uhuru.

Ø  Kuanzishwa kwa program za mafunzo ya wahudumu wa afya na madaktari

Ø  Serikali ilijitahidi kuleta vifaa tiba na dawa kutoka nje ya nchi ili kuongeza ubora wa huduma zilizokuwa zinatolewa.

v  Juhudi zote hizi ziliwezesha kuboresha hali ya afya kwa ujumla na kuweka mfumo wa afya wakushughulikia changamoto mbalimbali za kiafya.

 

UTAMADUNI NA MAADILI

Ø  Utamaduni ni mfumo wa maisha unaojengwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kupitia malezi, elimu na mawasiliano ndani ya jamii.

Ø  Utamaduni hujumuisha imani, maadili, mila na desturi, lugha, sanaa, muziki, mavazi chakula na tabia zinazoainisha kundi fulani.

Ø  Serikali baada ya uhuru ilifanya mambo yafuatayo ili kuimarisha utamaduni na maadili miongoni mwa Watanzania.

 

a)      Kuifanya lugha ya Kiswahili kuwa lugha rasmi ya taifa.

Kiswahili kilitumika kama njia ya kuhifadhi na kueneza maarifa, maadili na historia ya jamii

b)      Kuanzishwa kwa vyombo mbalimbali vya kusimamia sanaa na michezo ili kulinda na kukuza utamaduni wetu.

Ø  Mfano Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Baraza la Michezo Taifa (BMT), Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA),  Bodi ya Filamu Tanzania, Makumbusho ya taifa na vyama mbalimbali vya kusimamia michezo kama mpira wa miguu, pete, kikapu, ndondi na riadha

c)      Sanaa mbalimbali zilipewa kipaumbele kama vile uchoraji, uchongaji, ngoma na nyimbo.

d)      Miziki pia ilianzishwa, ambayo ilikuwa na lengo la kuelezea maadili na mapambano yaliyofanywa kulikomboa taifa

e)      Wasanii na waandishi wa vitabu walihimizwa kutumia kazi zao kuelimisha umma kuhusu ujenzi wa taifa.

 

MIKAKATI YA UJENZI WA TAIFA

Ø  Kati ya mwaka 1961 hadi 1966, serikali ya Tanzania iliweka mikakati mbalimbali ya kujenga taifa linalojitegemea. Mikakati hiyo ni kama ifuatayo:

i.      Kuanzishwa kwa mfumo wa chama kimoja cha siasa.

Chama cha TANU pamoja na ASP cha zanzibar ndivyo vilivyoruhusiwa kufanya shughuli za kisiasa. Lengo la kufanya hivyo ni kuleta umoja na mshikamano baina ya wananchi, kuondoa siasa za kibaguzi na kupunguza migogoro ya kisiasa.

ii.      Kuondolewa kwa mifumo ya uchifu katika uongozi wa nchi.

Lengo ilikuwa ni kulijenga taifa upya. Machifu walikuwa na nguvu kubwa katika jamii zao na mara nyingi walitumiwa na wakoloni kama vibaraka wao

iii.      Kuanzishwa kwa jeshi la kujenga taifa (JKT) tarehe 10 julai 1963.

Lengo ilikuwa ni kukuza uzalendo, maadili na ujenzi wa taifa. Jeshi hili lililenga kutoa mafunzo ya kijeshi pamoja na stadi za kazi kwa vijana wa kitanzania.

 

Baada ya miaka mitano ya uhuru wa Tanganyika, yaani 1966, vitendo vya rushwa vilionekana kuongezeka na baadhi ya viongozi wa umma walianza kujisahau.

 

Baadhi ya mambo yaliyojitokeza baada ya uhuru ni kama yafuatayo:

a) Kujengeka kwa matabaka ya kiuchumi, kisiasa na kijamii, kinyume na mfumo wa kijamii uliokuwepo kabla yauhuru ambapo jamii iliishi kwa umoja,udugu,upendo na kushirikiana

b) Baadhi ya viongozi na watumishi wa umma walianza kukiuka maadili ya utumishi wa umma na kutumia nafasi walizopewa kama vitega uchumi ili kujinufaisha wenyewe

 

Ø  Baada ya hayo kuanza kuonekana, serikali chini ya Mwalimu JK Nyerere iliunda tume ya Rais ya Kudumu ya Uchunguzi (The presidential Permanent Commission of Enquiry) ili kuchunguza mwenendo wa viongozi na watumishi wa umma waliokuwa wakikiuka maadili, kujilimbikizia mali na kutumia madaraka vibaya kinyume na miiko ya chama cha TANU.

 

 

CHANGAMOTO ZA UJENZI WA TAIFA

Ø  Kipindi cha mwaka 1961 hadi 1966 Taifa lilipitia changamoto mbalimbali za kiuchumi, kijamii na kisiasa. Mfano, matumizi ya zana duni na ukosefu wa wataalamu katika sekta ya kilimo,

 

Baadhi ya changamoto zilizoathiri ujenzi wa taifa mara baada ya uhuru ni kama ifuatavyo:

a)      Uasi wa jeshi mwaka 1964

Ø  Uasi wa januari 20-27, 1964 pale Lugalo, ambapo kikundi kidogo cha wanajeshi wa Tanganyika Rifles (TR) kiliasi na kutaka kuipindua serikali.

Ø  Jaribio hilo lilizimwa na waliohusika walipewa adhabu kali, kama kufukuzwa jeshini, kufungwa na kuwekwa kizuizini kwa muda mrefu.

Ø  Uasi huu ulisababisha kuundwa kwa jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ)

b)     Kuibuka kwa tabaka la mapepari uchwara

Ø  Kama ilivyokuwa katika nchi nyingine nyingi za Afrika, tabaka jipya la mabepari uchwara waliokuwa wamechukua madaraka serikalini walianza kutumia nyadhifa zao kujinufaisha.

Ø  Wananchi walianza kushuhudia viongozi wakiishi maisha ya anasa huku raia wa kawaida wakibaki masikini.

Ø  Hali hii ilikuwa tishio kwa umoja, maadili, amani na mshikamano uliokuwa unasisitizwa na kujengwa mara baada ya uhuru

c)      Hali mbaya ya uchumi

Ø  Katika kipindi hiki, hali mbaya ya uchumi ilitokea na kuathiri sana upatikanaji wa huduma za kijamii kama elimu, afya na nyinginezo zilizotolewa na serikali.

Ø  Tatizo hili lilisababisha pia ukosefu wa wataalamu , teknolojia duni, kuongezeka kwa maradhi, ujinga na umasikini, pamoja na kuwepo kwa miundombinu mibovu.

Ø  Hata hivyo serikali ilianza kuchukua hatua za mageuzi ili kurekebisha changamoto hizo

d)     Ukabila na migawanyiko ya kijamii

Ø  Kulikuwepo na makabila mengi yenye mila na desturi tofautitofauti. Hali hii ilileta changamoto katika kujenga umoja wa kitaifa, kuzuia siasa za kikabila n.k

e)      Changamoto au upungufu wa fedha.

Ø  Serikali mpya ilikuwa haina mapato ya kutosha hivyo kutegemea zaidi misaada ya nje. Hali hii ilipunguza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

f)       Elimu duni na ujinga.

Ø  Katika kipindi hiki, kiwango cha elimu kilikuwa cha chini sana kwakuwa shule zilikuwa chache na watu wengi hawakujua kusoma na kuandika. Hali hii iliathiri uelewa wa wananchi kuhusu maendeleo na utaifa.

g)      Athari za ukoloni

 

ZOEZI

1.      Eleza jinsi tabaka jipya la mabepari uchwara lilivyoathiri umoja na maadili ya kitaifa baada ya uhuru

2.      Fafanua mikakati iliyochukuliwa na serikali baada ya uasi wa jeshi wa januari 1964 ili kuimarisha usalama wa taifa

3.      Fafanua umuhimu wa sera na mifumo ya kisiasa iliyoanzishwa mara baada ya uhuru katika maendeleo ya kiuchumi na kisiasa kwa Tanzania ya sasa

4.      Eleza faida za Tanganyika kuwa jamhuri

5.      Ni maadili gani yalijengwa na kukuzwa wakati wa ujenzi wa taifa, 1961 hadi 1996?

6.      Ni njia gani bora zinazoweza kutumika kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa wakati wa sasa?

7.      Pendekeza mikakati ya kuendelea na ujenzi wa taifa la Tanzania wakati wa sasa

8.      Ni kwa jinsi gani ngoma na nyimbo za jadi zinaweza kutumika katika kujenga maadili na umoja wa kitaifa wakati wa sasa?


No comments:

Post a Comment